Msiipende dunia

Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake. Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia. Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele” (1 Yohana 2:15-17).

Mtume Yohana aliandika barua hii kwa kusudi fulani. Anasema kwamba, “Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu” (1 Yohana 5:13). Barua hii iliandikwa kwa wale “ambao wanaamini katika Jina la Mungu” Iliandikwa ili waweze kujua kwamba wako na uzima wa milele. Katika nchi yetu kuna wengi ambao wanadai kuwa wameokoka. Kila siku tunakutana na watu ambao wanasema mambo kama haya: “Bwana asifiwe, nimeokoka, Yesu ni Bwana wa maisha wangu.” Lakini Biblia inatuambia kwamba kuna watu ambao hudai wameokoka ilhali bado; wamejidanganya. Dhambi na shetani zimewadanganya kwa kujiwazia kwamba wameokoka ilhali bado. Hawa ni watu ambao Bwana Yesu Kristo alizungumzia akisema kwamba, “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe, ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu” (Mathayo 7:21-23).

Kwa hivyo tunaona kwamba mtu akisema ameokoka, basi ni lazima ahakikishe kwamba hajidanganyi. Ni lazima ahakikishe kwamba kweli ameokoka na siyo tu maneno matupu. Je, atawezaje kufanya hivi? Je, atajichunguza aje ili aweze kujua kwamba ako katika imani? (2 Wakorintho 13:5). Jibu ni kwamba anahitaji kusoma barua hii ambayo Yohana aliandika na achunguze maisha yake kulingana na yale ambayo Yohana aliandika. Tunaposoma barua hii, tunaona kwamba Yohana anatupatia mthihani. Tunafaa kuchunguza imani yetu na maisha yetu kulingana na maneno yake ili tuone kabisa kama tumeokoka au la.

Katika mafundisho haya tutatazama 1 Yohana 2:15-17. Hapa tunapata maagizo ili tuweze kuona kabisa kama tumeokoka au la. Kuna mambo matatu katika mistari hii.

1. Yohana anatuambia kwamba tusiipende dunia

Mtu ambaye ameokolewa kwa ukweli haupendi ulimwengu na vitu vyake. Anaishi katika ulimwengu na anatumia vitu vya ulimwengu huu, lakini moyo wake hauko katika vitu hivi. Akiwa na upendo wa vitu vya ulimwengu huu basi “upendo wa Baba haumo ndani mwake.”

Je, Yohana anamaanishi nini wakati anapozungumza kuhusu ulimwengu? Katika kifungu hiki Yohana anafafanua hivi kuhusu ulimwengu kwamba ulimwengu ni tamaa ya mwili, tamaa ya macho, majivuno ya mali. Mwili ndiyo kile Biblia inaita hali ya dhambi, hii ni hali ya kila mtu ambaye hajaokoka. Biblia inasema kwamba, “Kwa maana wale waufuatao mwili huyafikiri mambo ya mwili; bali wale waifuatao roho huyafikiri mambo ya roho. Kwa kuwa nia ya mwili ni mauti; bali nia ya roho ni uzima na amani. Kwa kuwa ile nia ya mwili ni uadui juu ya Mungu, kwa maana haitii sheria ya Mungu, wala haiwezi kuitii. Wale wafuatao mwili hawawezi kumpendeza Mungu” (Warumi 8:5-8).

Kile kwa hivyo Yohana anasema ni kwamba “dunia” ni vitu ambavyo viko katika dunia na vinatamanika na watu wa dunia na hao hujivuna kwa sababu ya vitu hivi. Wale ambao hawajaokoka wanapenda anasa na mali ya ulimwengu huu. Watu hawa hufanya kazi kwa bidii sana ili waweze kupata vitu hivi. Kwao mambo kumhusu Mungu si kitu. Labda unaweza kupata watu hawa huenda kanisani kila Jumapili, lakini mioyo yao haiko katika mambo ya Mungu, bali katika mambo ya ulimwengu huu. Watu hawa hupenda vyeo, mamlaka, heshima, pesa na mali. Haja yao ni kuwa na nyumba kubwa ya kifahari ili majirani na marafiki wao waweze kuwatamani. Haja yao pia ni kuwa na vyeo vya kuheshimika katika jamii ili watu waweze kuwaheshimu na kuwaomba usaidizi. Hivi ndivyo wale ambao hawajaokoka walivyo. Wanapenda vitu vya ulimwengu huu. Wanajiwekea hazina zao hapa ulimwenguni. Maisha yao yote inatawaliwa na vitu vya ulimwengu huu. Kuabudu Mungu si kitu kwao. Yesu alizungumza kuhusu watu hawa kwa kusema “Msijiwekee hazina duniani, nonda na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina mbinguni, kusikiharibika kitu kwa nonda wala kutu, wala wevi hawavunji wala hawaibi; kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako” (Mathayo 6:19-21).

Kwa hivyo katika kifungu hiki Yohana anasema kwamba wale wote ambao wameokoka hawafuati vitu vya ulimwengu huu: “Msiupende ulimwengu na vitu vyake.” Ikiwa mtu anapenda ulimwengu huu na vitu vyake, basi ni ishara tosha kwamba mtu huyo hajaokoka. Anaweza kujidai kwamba ameokoka, lakini jinsi anavyoishi maisha yake ni ishara tosha kwamba hajaokoka.

2. Yohana anatuambia sababu kwa nini tusiipende dunia

Anasema kwamba “Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia .” Kuna sababu mbili katika mistari hii kwa nini hatufai kuupenda ulimwengu.

(i) Kwa sababu yale yote ambayo yako katika ulimwengu huu hayatoki kwa Baba. Mungu ni mtakatifu na ndani mwake hamna dhambi. Kwa upande mwingine ulimwengu umejawa na dhambi. Ulimwengu uko katika upinzani na Mungu, umemwasi Mungu, unamchukia Mungu na neno lake na pia uko vitani na Mungu. “Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba.” Watu wale ambao hawajaokoka, hawajali kabisa mambo ya Mungu. Hawajali ufalme wa Mungu na kueneza injili yake ulimwenguni kote. Wanajali tu starehe zao na kutafuta starehe zao tu na anasa za ulimwengu huu. Hii ndiyo sababu Yakobo anasema kwamba “Kuwa rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu” (Yakobo 4:4).

(ii) Kwa sababu “Ulimwengu unapita na vitu vyake vyote.” Ulimwengu jinsi ulivyo hautakuwepo milele. Ulimwengu uko chini ya laana na siku moja utaharibiwa, na ulimwengu upya utaumbwa. Hii ni sababu hatufai kuupenda ulimwengu na vitu vyake vyote; kwa sababu siyo wa milele bali unapita.

3. Yohana anatuambia jambo kuhusu watu ambao wanapenda ulimwengu huu

Anasema kwamba, “Ikiwa mtu anapenda ulimwengu, upendo wa Baba hauko ndani mwake.” Katika msatari huu Yohana anasema kwamba ikiwa mtu anaupenda ulimwengu na kutafuta anasa za ulimwengu huu kwa sababu anatamani vitu vya ulimwengu kwa kupata furaha, basi upendo wa Baba hauko ndani mwake. Hii inamaanisha kwamba mtu huyo hajapokea upendo wa wokovu wa Baba moyoni mwake na pia kwamba hana upendo kwa Baba moyoni mwake. Biblia ianfunza kwamba tunaweza tu kupenda Mungu au vitu vya ulimwengu huu; hatuwezi kupenda Mungu na vitu vya ulimwengu huu pamoja. Yesu alisema kwamba, “Hakuna mtu awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia huyu na kumpenda huyu; ama atashikamana na huyu, na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali” (Mathayo 6:24).

Katika nchi yetu leo kuna watu wengi husema kwamba wameokoka. Lakini unapotazama maisha yao utapata kwamba wanapenda ulimwengu. Mara mingi mtu anaweza kusema kwamba, “Mtu huyo ameokoka, lakini amerudi nyuma katika wokovu wake; alikuwa akija kanisani kila Jumapili lakini sasa anapenda ulimwengu sana. Lakini ukweli ni kwamba tunajua ameokoka kwa sababu alimpokea Yesu.” Lakini Biblia haifundishi hivi. Biblia inasema kwamba ikiwa mtu ameokoka, ataishi maisha ya wokovu. Ikiwa mtu haishi maisha ya wokovu, basi ni ishara kwamba hajaokoka. Kwa hivyo katika kifungu hiki Yohana anasema kwamba, “Ikiwa mtu anapenda ulimwengu, upendo wa Baba hauko ndani mwake.” Kwa sababu anapenda ulimwengu na kutafuta vitu vya ulimwengu huu, ni ishara kwamba mtu huyo hajaokoka. Ikiwa mtu huyo angekuwa ameokoka, hangetafuta anasa na mali za ulimwengu huu. Badala yake atautafuta ufalme wa Mungu na utakatifu wake (Mathayo. 6:33).

Back to contents…

Print This Page Print This Page
Tags: , , , ,

Leave a Reply